GENERATION OF LOVE UNIT

GENERATION OF LOVE UNIT
GENERATION OF LOVE@2013

Wednesday, October 16, 2013

JANGWANI PANOGA, WAITWA WANACHAMA KUTOA UAMUZI WA MWISHO

Na. Frank Charles Gibebe
KLABU ya Yanga ya Dar es Salaam imepiga hatua katika mchakato wa kuanzisha kampuni kwa kuanza rasmi mchakato wa kupigisha kura wanachamwa wake kuunga mkono au kupinga wazo hilo.
Kaimu Katibu Mkuu wa Yanga SC, Lawrence Mwalusako amesema leo asubuhi katika Mkutano na Waandishi wa Habari makao makuu ya klabu, Jangwani, Dar es Salaam kwamba wanachama watatakiwa kufika makao makuu ya klabu kupiga kura zao.
Kaimu Katibu Mkuu wa Yanga SC, Lawrcence Mwalusako kulia akizungumza na Waandishi wa Habari leo makao makuu ya klabu. Kushoto ni Ofisa Habari wa klabu, Baraka Kizuguto.

Mwalusako alisema kwamba kwa wanachama wa mikoani wataandaliwa utaratibu maalum wa kushiriki zoezi hilo.
Katika Mkutano wa Kawaida wa Wanachama wa Yanga uliofanyika tarehe 16 Januari 2013 Mwenyekiti kwa niaba ya Kamati ya Utendaji aliwapa Wanachama wafikirie mapendekezo ya YANGA kuwa Kampuni ama kutokuwa Kampuni kisha kuyawasilisha kwa Katibu Mkuu wa klabu.
“Nachukua nafasi hii kuwaambia Wanachama wa Yanga kuwa kuanzia leo tarehe 16 Oktoba 2013 mpaka tarehe 10 Novemba 2013, kutakuwa na sanduku moja hapa klabuni kwa ajili ya kukusanya kura za maoni ya wanachama ya kuanzisha kampuni (NDIYO) au kutokuwa Kampuni (HAPANA),”alisema Mwalusako.
Mwalusako alisema kila mwanachama hai atakuwa na uhuru wa kupiga kura na atalazimika kufika na kadi yake makao makuu ya klabu, ambapo itamzuia kupiga kura mara mbili au zaidi.
Yanga SC ilianzishwa mwaka 1935 na kwa wakati wote huo imekuwa katika mfumo wa klabu, ingawa mara kadhaa kuanzia miaka ya 1990 yalifanyika majaribio ya kuigeuza kampuni bila mafanikio na kusababisha hadi migogoro mikubwa.
Chini ya Uenyekiti wa Alhaj Yussuf Mehboob Manji, aliyeingia madarakani Julai 15, mwaka jana, Yanga SC inajaribu tena kutimiza ndoto zake za kujiendesha katika mfumo mpya wa kampuni. 

No comments:

Post a Comment